Monday, November 16, 2015

SHULE YA KIMATAIFA IRINGA YAFANYA SIKU YAKE YA KIMATAIFA, YASHAURI MABORESHO KATIKA SEKTA YA ELIMU





SHULE ya Kimataifa ya Iringa imetoa wito kwa serikali ya Dk John Magufuli kuanzisha mpango maalumu wa uingizaji na utumiaji wa teknolojia mbalimbali mpya kwa maendeleo ya nchi kwa kutoa ufadhili wa elimu kwa makundi mbalimbali ya wanafunzi watakaoplekwa katika nchi zenye teknolojia hizo.

Pamoja na mpango huo, shule hiyo imeiomba serikali hiyo kutumia utajiri wa gesi ya Mtwara kuendelea kuboresha mazingira na mifumo ya utoaji wa elimu nchini ili iwiane na nchi zilizopiga hatua kubwa katika sekta hiyo.

Hayo yalisemwa na mjumbe wa bodi ya shule hiyo, Edwin Porch kwenye maadhimisho ya siku ya kimataifa ya shule hiyo yenye wanafunzi wa shule ya msingi na sekondari zaidi ya 100, yaliyofanyika shuleni hapo juzi.

Mkuu wa Utawala wa shule hiyo, Jean Milliken alisema; “Kwasababu shule yetu ni ya kimataifa, tumekuwa na kawaida kila mwaka kuwa na siku hii, tunasheherekea utaifa wetu kwasababu tunatoka mataifa mbalimbali.”

Milliken alisema kwa kupitia siku hiyo; wafanyakazi, wanafunzi na wazazi na walezi wao hufanya sherehe kwa kuonesha tamaduni za nchi wanazotoka vikiwemo vyakula vinavyoliwa na mataifa hayo na kufanya maonesho mbalimbali yenye maudhui ya kukuza sekta ya elimu nchini.

Akizungumzia sekta ya elimu na matumizi ya teknolojia kwa maendeleo ya Taifa, Porch alisema; “nchi inahitaji shule nyingi za vipaji maalumu sambamba na zile za kimataiafa ili zitoe wataalamu wengi kwa faida ya nchi .”

Alisema mazingira ya Tanzania yanaruhusu kufanyika kwa mapinduzi makubwa ya kiuchumi kama uwekezaji wa kutosha utafanywa katika sekta ya elimu.

“Tanzania inaweza kuwa kama Japan ambayo leo imepiga hatua kubwa ya maendeleo duniani baada ya kuwapeleka watu wake katika nchi mbalimbali duniani ambako walijifunza na kurudisha kwao tekenolojia zilizoliofanya taifa hilo liwe moja kati ya nchi zilizoendelea kiviwanda,” alisema.

Alisema wakati Japan ikipeleka watu wake katika nchi zingine zilizoendelea kujifunza tekenolojia za huko haikuwa mzalishaji mkubwa wa magari lakini hivi sasa; magari yake yanauzwa kila nchi duniani.

Alisema Tanzania inaweza kuwa nchi ya viwanda vinavyotokana na matumizi ya tekenolojia zake kama itathubutu kufanya kile kilichofanywa na Japan.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini, Salim Asas alisifia uwepo wa shule hiyo ya kimataiafa mjini Iringa akisema unasaidia kuupaishia mkoa wa Iringa katika utoaji wa elimu ya kimataifa.

Alisema serikali ina kila sababu ya kuzisaidia shule za kimataifa ili zichukue wanafunzi wengi zaidi wa kitanzania lakini pia zivutie wageni toka nje ya nchi.

Asas alisema elimu inayotolewa katika shule za kimataifa ni elimu bora inayowaandaa wanafunzi kushindana kimataifa katika nchi yoyote ile duniani jambo ni sifa na ni maendeleo kwa nchi.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More