Sunday, November 29, 2015

Maamuzi Mapya ya Rais Magufuli Kuhusu Serikali Kupunguza Matumizi ya Fedha Ikiwemo za Kalenda na Diaries

Katibu  Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue ametoa ufafanizi wa maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John  Pombe Magufuli kuhusu kupunguza matumizi yasiyo ya lazima katika Wizara,idara na Taasisi za serikali.

Katika ufafanuzi huo,Balozi Sefue amemtaka kila Mtendaji Mkuu ama Afisa Masuhuli wa serikali kujiuliza mwenyewe ni kwa kiasi gani anatekeleza kwa vitendo nia ya Rais ya kuepuka matumizi yasiyo ya lazima

"Rais ameonesha njia, sasa kwa wakati huu ni vema kila mtendaji mkuu wa serikali,ajiulize endapo Rais atafika katika eneo langu la kazi,ni kwa kiasi gani atakuta nimetekeleza maagizo yake?" Amesisitiza Balozi Sefue

Kutokana na ufafanuzi huo, Blozi Sefue pia amezungumzia uchapishaji wa kalenda na vitabu vya kumbukumbu yani  "Diaries" akisema kila mtendaji mkuu wa Serikali ama Afisa Masuhuli apime mwenyewe kama ni lazima kutengeneza au kuchapisha kalenda na Diary? na kama ni lazima achapishe kwa kiasi gani?

"Ni matumizi mabaya ya fedha za umma kwa kila wizara,Idara na Taasisi za serikali kuchapisha idadi kubwa ya kalenda na Diaries ambazo wakati mwingine hata hazitumiki mpaka mwaka unakwisha." Ameongeza Balozi Sefue

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es Salaam  Novemba 28,2015

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More