Friday, November 27, 2015

MHAKAMA YA MAFISADI MBIONI KUANZA KUHUKUMU

Utekelezaji wa ahadi za Rais John Magufuli unazidi kushika kasi baada ya kuanza kwa mchakato wa kuanzisha mahakama maalumu ya kuwashughulikia mafisadi.
 
Jaji Kiongozi, Shaban Lila alisema jana kuwa tayari wadau mbalimbali wa haki jinai wameanza kukutana kuangalia namna ya kuanzisha mahakama hiyo kama sehemu ya utekejezaji wa ahadi ya Rais.
 
Akizungumza katika hafla ya kuhitimisha mafunzo ya kushughulikia mashauri nyeti ya jinai kwa majaji 12 wa Mahakama Kuu ya Tanzania, alisema juzi walikuwa na mazungumzo na Wizara ya Katiba na Sheria kuangalia mfumo wa uendeshaji wa mahakama hiyo.
 
“Tunaangalia tuianzishe kama mahakama huru au ifanywe ndani ya muundo wetu wa mahakama kwa kuipa kipaumbele maalumu. Lakini tunafikiria zaidi kama ingekuwa ni kitengo maalumu ndani ya Mahakama Kuu kitakachokuwa kikishughulikia mafisadi,” alisema Jaji Lila.
 
Hata hivyo, Jaji Lila hakutaja muda maalumu utakaotumika kumaliza mchakato wa kuanzisha mahakama hiyo, huku akisema unahusisha wadau wengi na unyeti wake unahitaji maandalizi makubwa. 

Jaji huyo bila kutaja takwimu, alieleza kuwa kesi za makosa makubwa ya jinai zinaongezeka nchini ukilinganisha na miaka ya nyuma hasa zile zinazohusu utakatishaji fedha, ugaidi, usafirishaji wa dawa za kulevya, usafirishaji wa nyara za Serikali hasa wanyama hai na mazao yake na ufisadi.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More