Dkt. Msowoya aliwahimiza wanafunzi kuipenda nchi yao, kusoma kwa bidii na kuepuka makundi yenye viashiria hasi katika masomo na maisha kwa ujumla.
Dkt. Msowoya aliwahimiza wanafunzi kuipenda nchi yao, kusoma kwa bidii na kuepuka makundi yenye viashiria hasi katika masomo na maisha kwa ujumla.
Wananchi wanaozunguka Shamba la Miti Sao Hill wameendelea kunufaika kielimu na kiuchumi kupitia ushiriki wao katika shughuli za uchukuaji miche ya miti zinazofanyika katika bustani za miche zilizopo Tarafa ya Kwanza Irundi na Tarafa ya Tatu Ihalimba.
Shughuli hizo ni sehemu ya mpango endelevu wa upandaji miti unaotekelezwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa lengo la kuendeleza misitu ya kupandwa, kuongeza uzalishaji wa rasilimali za misitu na kuimarisha uhifadhi wa mazingira.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Msaidizi wa Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Said Singano, alisema uchukuaji wa miche unafanyika kwa kuzingatia taratibu na kanuni za kitaalamu ili kulinda ubora wa miche.
“Tunasisitiza miche ichukuliwe kwa uangalifu mkubwa ili isiharibu mizizi, kwa sababu ubora wa miche ndiyo msingi wa mafanikio ya upandaji miti mashambani,” alisema Singano.
Shughuli hizo pia zimeongeza uelewa wa wananchi kuhusu mchango wa Shamba la Miti Sao Hill katika uhifadhi wa mazingira, mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na upatikanaji endelevu wa mazao ya misitu kwa manufaa ya Taifa.
Mmoja wa wananchi walioshiriki zoezi hilo, Bw. Joshua Ng'umbi kutoka Kijiji cha Igowole Wilaya ya Mufindi, alisema ushiriki wake umemsaidia kuongeza kipato na kupata ujuzi mpya katika shughuli za misitu.
“Mbali na kupata ajira, nimejifunza kuchagua miche bora na namna sahihi ya kupanda miti ili iweze kuota vizuri na kukua kwa ubora unaoweza kuleta kipato kizuri wakati wa uvunaji,” alisema Bw. Joshua.
Kwa ujumla, zoezi la uchukuaji miche katika Tarafa za Irundi na Ihalimba limeendelea kuleta manufaa makubwa kwa Shamba la Miti Sao Hill na wananchi kwa kuimarisha juhudi za upandaji miti, kutoa ajira na kukuza uelewa wa masuala ya misitu na uhifadhi wa mazingira.
Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Hassan Ngoma aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea katika hafla ya kukabidhi kisima cha maji kilichojengwa na RUNALI katika kituo cha afya Marambo kwa uongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Nachingwea
Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Hassan Ngoma aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea akifungua maji wakati hafla ya kukabidhi kisima cha maji kilichojengwa na RUNALI katika kituo cha afya Marambo kwa uongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Nachingwea Na Fredy Mgunda, Nachingwea
Chama Kikuu cha Ushirika RUNALI kimetatua changamoto ya upatikanaji wa maji katika Kituo cha Afya Marambo, changamoto iliyodumu kwa miaka mingi na kusababisha baadhi ya huduma kushindwa kutolewa ipasavyo katika kituo hicho.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kisima hicho cha maji, Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika RUNALI, Odas Mpunga, alisema kuwa lengo kuu la mradi huo ni kusogeza huduma muhimu kwa jamii inayohudumiwa na Kituo cha Afya Marambo.
Mpunga alisema chama hicho kilipokea maombi ya kusaidia kutatua changamoto ya maji katika kituo hicho cha afya, hali iliyopelekea RUNALI kuchukua jukumu hilo kwa dhamira ya kuisaidia jamii.
Aliongeza kuwa kisima hicho kimekamilika na kuanza kutoa huduma, hivyo ni jukumu la wananchi pamoja na viongozi wa eneo hilo kuhakikisha wanakitunza ili kiwe mradi endelevu wenye manufaa ya muda mrefu.
Kwa upande wake, Meneja wa RUNALI, Jahida Hassan, alisema kuwa utekelezaji wa mradi huo ni sehemu ya kutimiza msingi wa saba (7) wa vyama vya ushirika, unaohimiza vyama hivyo kurudisha mchango kwa jamii inayowazunguka.
Jahida aliongeza kuwa kisima hicho ni kirefu na kina maji ya kutosha, hivyo kinapaswa kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa, hususan kuhudumia Kituo cha Afya Marambo.
Alisema kuwa RUNALI imetumia zaidi ya shilingi milioni 15 kuchimba kisima hicho hadi kukamilika kwake na kuanza kutoa huduma za maji katika kituo hicho cha afya.
Naye mgeni rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, Hassan Ngoma, aliwataka wananchi na viongozi wa eneo hilo kuhakikisha wanauhudumia na kuutunza mradi huo ili uwe na manufaa ya kudumu kwa jamii na serikali kwa ujumla.
Ngoma alisema kuwa fedha nyingi zimewekezwa katika mradi huo wa kisima cha maji kwa lengo la kutatua kero ya maji kwa wagonjwa, wahudumu wa afya pamoja na wananchi wanaohudumiwa na kituo hicho, hivyo ni muhimu kulinda na kuutunza uwekezaji huo.
Aidha, aliwahimiza wananchi na wakulima ambao bado hawajajiunga na vyama vya ushirika kufanya hivyo kwa ajili ya maendeleo yao binafsi na maendeleo ya taifa kwa ujumla.
Wajumbe wa Baraza la OSHA wakiimba wimbo wa mshikamano (solidarity) wakati wa kikao cha Tano cha Baraza la Tano la wafanyakazi wa OSHA kilichofanyika katika Ofisi za OSHA Jijini Dodoma Desemba, 20, 2025Wajumbe wa Baraza la OSHA wakifuatilia majadiliano mbalimbali yaliowasilishwa katika kikaocha Tano cha Baraza la Tano la wafanyakazi wa OSHA kilichofanyika katika Ofisi za OSHA Jijini Dodoma.Desemba, 20, 2025.Na Fredy Mgunda
Katibu Mkuu katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano ya Kazi), Bi. Mary Maganga, amesema Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) ni taasisi yenye umuhimu mkubwa katika kuwezesha shughuli za uzalishaji kufanyika kwa tija na ufanisi.
Bi. Maganga ametoa kauli hiyo wakati akifungua Kikao cha Tano cha Baraza la Tano la Wafanyakazi wa OSHA kilichofanyika leo, Desemba 20, 2025, jijini Dodoma, ambapo alikuwa mgeni rasmi.
Amesema OSHA ina jukumu muhimu la kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi, huku akiipongeza taasisi hiyo kwa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Aidha, amewasisitiza watumishi kuendelea kufanya kazi kwa weledi, kuzingatia kanuni za utumishi wa umma na kuimarisha ushirikiano kazini.
“Kabla ya kufungua rasmi kikao hiki, napenda kusisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa weledi. Mara nyingi tumekuwa tukiamini kuwa wito unawahusu zaidi viongozi wa dini, lakini hata kazi zetu hizi ni wito, kwani kuna wananchi wengi wanaotegemea huduma zetu,” amesema Bi. Maganga.
Awali, akimkaribisha Katibu Mkuu kufungua kikao hicho, Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, amesema kikao hicho kinalenga kutathmini utendaji wa taasisi kwa kipindi kilichopita na cha sasa, pamoja na kuweka mwelekeo wa maendeleo ya OSHA kwa kipindi kijacho.
Amesema kikao hicho kinatazama utekelezaji wa shughuli za mwaka wa fedha 2024/2025 pamoja na tathmini ya utendaji katika miezi mitano ya mwaka wa fedha 2025/2026, ikiwa ni maandalizi ya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027.
Bi. Mwenda ameongeza kuwa kikao hicho kilitanguliwa na mafunzo kwa watumishi wote wa OSHA yaliyohusu maadili ya utumishi wa umma, mpango mkakati wa taasisi wa miaka mitano ijayo (2026/2027–2030/2031), masuala ya afya ya akili na itifaki.
Kwa upande wake, akitoa salamu za wafanyakazi, Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya (TUGHE), Bw. Rugemalila Rutatina, ameipongeza OSHA kwa kuzingatia ushirikishwaji wa watumishi wote bila ubaguzi katika kufanya maamuzi yanayohusu utendaji wa taasisi hiyo.
Na Fredy Mgunda.
Afisa Tarafa ya Katerero, Bwanku M. Bwanku, ameshauri Meli mpya ya MV Mwanza kupitishwa katika Bandari ya Kemondo na nauli zake kupunguzwa ili wananchi wengi waweze kunufaika na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali ya Tanzania.
Bwanku alitoa ushauri huo umetolewa wakati wa kikao cha wadau wa bandari za Kagera kilichowakutanisha Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Kampuni ya Meli Tanzania (TASHICO) pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya usafiri wa majini.
Kikao hicho kililenga kupokea na kujadili maoni ya wadau kuhusu nauli za Meli mpya ya MV Mwanza, kikao kilichofanyika katika Hoteli ya ELCT mjini Bukoba.
Meli ya MV Mwanza ni meli kubwa na ya kisasa iliyojengwa kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 120, ikiwa na uwezo wa kubeba tani 400 za mizigo pamoja na abiria 1,200 kwa safari moja. Meli hiyo inatarajiwa kuanza safari zake rasmi katika Ziwa Victoria, ikihudumia mikoa ya Mwanza, Kagera na maeneo mengine ya ukanda wa Ziwa hivi karibuni.
Akizungumza katika kikao hicho, Bwanku alieleza kuwa licha ya mapendekezo ya awali ya TASAC na TASHICO kuwa meli hiyo itafanya safari kati ya Mwanza na Bukoba pekee, ni muhimu pia ipitie Bandari ya Kemondo ili kuongeza fursa za kiuchumi kwa wananchi wa maeneo ya jirani.
Aidha, alisisitiza umuhimu wa kupunguza nauli za meli hiyo ili wananchi wa kawaida waweze kumudu gharama za usafiri na hivyo kunufaika moja kwa moja na uwekezaji huo wa Serikali.
Kikao hicho kilifunguliwa na Mkuu wa Mkoa wa Kagera kupitia kwa Mkuu wa Wilaya ya Missenyi, Kanali (Mst) Hamis Maiga, ambaye aliwataka wadau kutoa maoni yao kwa lengo la kuboresha huduma za usafiri wa majini katika Ziwa Victoria.
Na Fredy Mgunda, Mufindi Iringa
Wahifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kutoka Shamba la Miti Sao Hill wamepatiwa mafunzo maalumu kuhusu masuala ya afya, yakilenga kuongeza uelewa juu ya maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) pamoja na magonjwa yasiyoambukiza, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha ustawi wao na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya uhifadhi wa misitu.
Mafunzo hayo yamelenga kuwaelimisha wahifadhi kuhusu hali halisi ya maambukizi ya VVU, njia za kujikinga, umuhimu wa upimaji wa hiari na wa siri, pamoja na kuondoa dhana potofu zinazokwamisha juhudi za kudhibiti maambukizi. Washiriki walikumbushwa kuzingatia maadili, kujilinda na kuchukua tahadhari stahiki katika maisha ya kila siku.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu, amesema mafunzo hayo hutolewa kila mwaka kama sehemu ya mafunzo endelevu kwa watumishi wa TFS, yakilenga kuwajengea uwezo wa kujikinga na magonjwa yanayoathiri afya na kushusha kasi ya utendaji kazi.
“Afya njema ni mtaji muhimu katika kulinda rasilimali za misitu, kwani kazi ya uhifadhi inahitaji nguvu, umakini na utayari wa mwili na akili. Ni muhimu kuzingatia maelekezo ya wataalamu ili kujikinga na magonjwa mbalimbali,” amesema PCO Yoramu.
Katika mafunzo hayo, mada za magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo na saratani zilijadiliwa kwa kina. Wahifadhi walielimishwa kuhusu dalili za awali, visababishi na athari za magonjwa hayo kwa afya na ufanisi wa kazi.
Washiriki walihimizwa kubadili mtindo wa maisha kwa kuzingatia lishe bora, kufanya mazoezi ya mara kwa mara, kudhibiti msongo wa mawazo na kuepuka matumizi ya pombe kupita kiasi pamoja na uvutaji wa sigara, ambavyo vimetajwa kuwa miongoni mwa vyanzo vikuu vya magonjwa yasiyoambukiza.
Naye Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga, Dkt. Bonaventura Chitopela, amesema kila mmoja ana wajibu wa kulinda afya yake kwa kupima afya mapema na kufuata ushauri wa wataalamu ili kupata matibabu kwa wakati.
“Tumia fursa hizi kupima afya zenu mara kwa mara ili kujua hali za kiafya mapema, hatua itakayowezesha kupata matibabu na ushauri kwa wakati,” amesema Dkt. Chitopela.
Kwa upande wake, Mkufunzi kutoka TACAIDS na Meneja wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Bw. Emmanuel Petro, amewataka wahifadhi kutumia kikamilifu elimu waliyoipata kwa kuchukua hatua za mapema dhidi ya changamoto za kiafya, akisisitiza kuwa uzingatiaji wa maelekezo ya wataalamu ni msingi wa kuzuia madhara ya kiafya.
Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za TFS kuhakikisha wahifadhi na watumishi wake wanakuwa na afya bora, nidhamu na uwajibikaji. Wahifadhi walioshiriki wameahidi kuzingatia elimu waliyoipata na kuwa mabalozi wa afya njema katika maeneo yao ya kazi na jamii zinazowazunguka.
Mbunge wa Jimbo la Nachingwea, Fadhili Liwaka,akisonga ugali kwenye moja ya masoko ambayo mama nitilie wanaojihusisha na uuzaji wa vyakulaNa Fredy Mgunda, Nachingwea.
Mbunge wa Jimbo la Nachingwea, Fadhili Liwaka, amewahakikishia mama lishe wa jimbo hilo kuwa atashughulikia changamoto zinazowakabili zikiwemo upatikanaji wa maji safi, usafi wa masoko, mikopo kwa wajasiriamali wadogo pamoja na maboresho ya miundombinu ya masoko ili yawe rafiki kwa wafanyabiashara na wateja.
Mheshimiwa Liwaka ametoa ahadi hiyo wakati wa ziara ya mikutano mbalimbali na mamalishe katika Kata za Nachingwea na Ugawaji, ikiwa ni sehemu ya jitihada zake za kuimarisha ushirikiano na kusikiliza kero zao moja kwa moja.
Akizungumza katika Soko Kuu la Nachingwea, Mbunge Liwaka alisema ameanza ziara zake kwa wajasiriamali wadogo kutokana na kutambua mchango wao mkubwa katika kuendesha uchumi wa familia na jamii kwa ujumla. Alisisitiza kuwa mamalishe ni nguzo muhimu ya uchumi wa chini, hivyo wanastahili kupewa kipaumbele.
“Ni wajibu wangu kuwa karibu nanyi, kuwashukuru kwa kuniunga mkono katika Uchaguzi Mkuu na kuomba ushirikiano wenu katika kuendelea kulijenga Jimbo la Nachingwea,” alisema Mheshimiwa Liwaka.
Kwa upande wake, mmoja wa mamalishe wa Soko la Voda, Bi. Fortunata Robert Makarius, alimpongeza Mbunge huyo kwa kuwafuata uso kwa uso, akisema hatua hiyo imewapa faraja na matumaini makubwa kwani haijawahi kufanywa na mbunge yeyote aliyewahi kuliongoza jimbo hilo.
Mbunge Liwaka alimalizia kwa kuwahakikishia mamalishe kuwa Serikali ya Wilaya kwa kushirikiana na Halmashauri itaendelea kushughulikia changamoto zao kwa hatua, huku akisisitiza mshikamano na ushirikiano kama msingi muhimu wa maendeleo ya Jimbo la Nachingwea.
Na Fredy Mgunda,Kilwa Lindi.
Mkuu wa Wilaya ya Kilwa, Mhe. Mohamed Nyundo, amewasimamisha kazi viongozi wa Serikali ya Kijiji cha Nanjirinji A, Kata ya Nanjirinji, ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za ugawaji na uuzaji wa ardhi kinyume cha utaratibu pamoja na matumizi mabaya ya mali za umma.
Hatua hiyo imechukuliwa baada ya wananchi kuwasilisha malalamiko mbele ya Mkuu wa Wilaya, wakimtuhumu Mwenyekiti Hamadi Makakala na Mtendaji Mbaruku Malukula kwa kufanya maamuzi makubwa bila kuwashirikisha wanajamii, kinyume na misingi ya utawala bora.
Akizungumza baada ya kusikiliza malalamiko hayo, DC Nyundo alisema kuwa ameunda kamati maalumu ya uchunguzi itakayopitia tuhuma hizo kwa kina na kutoa mapendekezo yatakayoiwezesha Serikali kuchukua hatua stahiki.
“Hatutaacha mwanya kwa mtu yeyote kutumia madaraka vibaya au kudhulumu rasilimali za wananchi. Uchunguzi utafanyika kwa uwazi na hatua kali zitachukuliwa kulingana na matokeo,” alisema Nyundo.
Ameongeza kuwa wananchi wanapaswa kuwa waangalifu dhidi ya taarifa zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii, akiwataka kutegemea vyanzo vya uhakika ili kuepuka kupotoshwa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Hemed Magaro, alitoa ufafanuzi kuhusu utofauti kati ya kuuza ardhi na kugawa ardhi kwa utaratibu maalumu, akisisitiza kuwa ardhi ya kijiji haiwezi kuuzwa bila kufuata sheria, taratibu na ridhaa ya mkutano mkuu wa kijiji.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, ameipongeza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa kazi ya kulinda rasilimali za misitu na nyuki, huku akiutaka wakala huo kuongeza kasi ya kutoa elimu ya uhifadhi kwa wananchi ili kukabiliana na changamoto za kimazingira zinazoongezeka nchini.
Ametoa wito huo wakati wa ziara yake katika Shamba la Miti Sao Hill, wilayani Mufindi, akiwa ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Dkt. Linda Salekwa, na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya hiyo.
Akizungumza na wahifadhi, Mkuu wa Mkoa amesema nidhamu na weledi ndani ya TFS ni sharti kuzingatiwa ili kuhakikisha sera na taratibu za uhifadhi zinatekelezwa kikamilifu.
“Nidhamu ni msingi wa ufanisi. Kama wahifadhi wa misitu yetu, ni lazima mjikite kwenye uwajibikaji na kutanguliza maslahi ya Taifa,” amesema James.
Amesifu uhusiano mzuri baina ya TFS na wananchi wanaoishi pembezoni mwa shamba hilo, akisema ushirikiano huo unaimarisha ulinzi wa misitu na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa rasilimali hizo.
“Kulinda misitu ni jukumu la Taifa zima. Endeleeni kutoa elimu mara kwa mara ili jamii ielewe kuwa misitu ni uchumi, ni mazingira, na ni uhai,” amesema.
Mhe. James ametahadharisha kuwa ukame unaoikumba nchi katika miaka ya hivi karibuni unachangiwa kwa kiasi kikubwa na uharibifu wa misitu, hali inayosababisha kupungua kwa mvua na kuongezeka kwa joto.
“Ukame unaongezeka kwa sababu tumeshindwa kuhifadhi misitu. TFS iendelee kuhamasisha upandaji na utunzaji wa miti bila kuchoka,” amesisitiza.
Awali, Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Dkt. Linda Salekwa, amesema Shamba la Miti Sao Hill limekuwa msaada mkubwa kwa jamii kwa kushiriki miradi mbalimbali ya maendeleo.
“TFS imetoa madawati, kujenga madarasa, mabweni, bwalo la chakula na kuendelea kusaidia jamii kwenye miradi ya kijamii. Ni taasisi inayowajibika,” amesema.
Kwa upande wake, Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu, amesema TFS imeendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kuhakikisha misitu inatumika kwa manufaa bila kuhatarisha uendelevu.
Ametaja shughuli zinazotekelezwa kuwa ni pamoja na ufugaji nyuki, uvunaji wa utomvu, uvunaji endelevu wa miti, na utoaji wa elimu kwa wananchi wa maeneo jirani.

