Tuesday, April 26, 2016

Mchina Ahukumiwa Miaka Mitatu Jela Kwa Kuuza Bidhaa Bila Kutoa Risiti

Mahakama ya Wilaya ya Ilala imemhukumu kifungo cha miaka mitatu jela au kulipa faini ya Sh4.5 milioni, mfanyabiashara Huifang Ma baada ya kupatikana na hatia ya kuuza bidhaa na kushindwa kutoa risiti kwa kutumia mashine ya kieletroniki. 
 
Ma ambaye ni raia wa China na mkazi wa Mtaa wa Narung’ombe eneo la Kariakoo, alihukumiwa kifungo hicho baada ya kukiri mashtaka mawili yaliyokuwa yakimkabili likiwamo la kushindwa kujisajili kulipa kodi ya ongezeko la thamani (Vat). 
 
Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mkazi Mwanadamizi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Said Mkasiwa alisema kwa kuwa mshtakiwa alikiri mashtaka yanayomkabili, anatakiwa kulipa faini au kwenda jela miaka mitatu. Hata hivyo, Ma alilipa faini na kuachiwa huru. 
 
Katika hati ya mashtaka, ilidaiwa kuwa Machi 23, mwaka huu eneo la Karikaoo, mshtakiwa alishindwa kutoa risiti za kieletroniki kwa mteja wake. 
 
Ilidaiwa kuwa siku hiyo mshtakiwa ambaye ni mmiliki wa Kampuni ya HM Textile Co Ltd iliyopo Mtaa wa Agrey, Kariakoo, alishindwa kutumia mashine za EFDs kwa ajili ya kutoa risiti kwa wateja walionunua bidhaa dukani kwake.
 
Kosa la pili, mshtakiwa alishindwa kujisajili kama mlipa kodi wakati akijua kufanya hivyo ni kosa kisheria.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More