Sunday, April 24, 2016

Kilimanjaro: Watumishi HEWA Wakopa Mamilioni ya Pesa Benki

Msako ulioanzishwa na Rais John Magufuli wa kutokomeza tatizo la wafanyakazi hewa katika utumishi wa umma, umeendelea kuibua mazito, ambapo mkoani Kilimanjaro, Benki ya CRDB imejikuta ikitoa mkopo kwa waliokuwa wafanyakazi hewa.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai, Helga Mchomvu aliyasema hayo akidai kuwa, yamegundulika baada ya Serikali kuunda kamati za uchunguzi wa tuhuma za ubadhirifu wa zaidi ya Sh milioni 500 katika halmashauri hiyo.

Kabla ya kuibuka kwa kisa hicho kinachoonesha namna wafanyakazi hewa alivyokuwa wakiibia nchi, hivi karibuni mkoani Singida, Mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Imani Nyamangaro, alipandishwa kizimbani akidaiwa kujilipa mishahara ya wastaafu 57, yenye thamani ya Sh milioni 29.4.

Mbali na mhasibu huyo, Rais Magufuli alipokuwa mapumziko kijijini kwake Mlimani, katika Wilaya ya Chato mkoani Geita, alieleza kisa kingine kilichoshitua jamii kuwa katika Mamlaka ya Mapato (TRA), kulikuwa na mtumishi mmoja ambaye alikuwa akilipwa mishahara ya watu 17.

Benki ya CRDB Hai
Akizungumza jana, Mchomvu alidai kuwa watumishi watatu wa halmashauri hiyo; wawili wa Idara ya Utumishi na mmoja Mchumi, walikopa katika Benki ya CRDB Sh milioni 35.2, kwa kutumia majina ya wafanyakazi hewa.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mkuu Idara ya Utumishi na Utawala, Gudila Mashele, Ofisa Utumishi Daraja la Kwanza, Faraja Ndatu na Mchumi Daraja la Pili, Isaiah Bayege. 
Kutokana na tuhuma hiyo iliyoibuliwa na kamati hizo za uchunguzi, Mchomvu alisema Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Hai, limewafukuza kazi watumishi hao.

Mbali na tuhuma ya kujipatia mkopo kwa kutumia majina ya wafanyakazi hewa, Mchomvu alisema kuna watumishi wengine wamefukuzwa kazi kwa tuhuma za wizi wa fedha za muda wa kazi wa ziada wa madaktari na wauguzi katika Hospitali ya Machame wilayani hapa, huku mwingine akifukuzwa kwa kununua dawa hewa za hospitali hiyo.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mhasibu Daraja la Kwanza, Edwin Kalokola na Mhasibu Msaidizi, Valentina Elisha, wanaodaiwa kuiba Sh milioni 24.4 za muda wa kazi wa ziada wa madaktari na wauguzi katika hospitali hiyo.

Mbali na wahasibu hao, yupo pia dereva Derick Urassa, aliyefukuzwa kwa tuhuma za kushiriki katika ununuzi wa dawa hewa katika hospitali hiyo zenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 32.7. 
Walioshushwa cheo  Alisema wapo pia watumishi walioshushwa vyeo kutokana na tuhuma mbalimbali, ikiwemo kughushi nyaraka na kuidhinisha malipo bila idhini ya mwajiri.

Miongoni mwao ni pamoja na Ofisa Muuguzi Msaidizi Daraja la Kwanza, Agness Chami na Katibu wa Afya Daraja la Kwanza, Gilbert Mashamba.

Wengine ni wahasibu waandamizi wawili, Kasisim Herpa na John Bogohe na Mhasibu Daraja la Kwanza, Christopher Manzi, ambao wanatuhumiwa kuidhinisha malipo mbalimbali ya Sh milioni 488.2, bila kuwa na idhini kinyume na taratibu za kazi.

Walivyobambwa Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Saidi Mderu alisema tuhuma hizo ziligunduliwa na Mkaguzi wa Ndani wa halmashauri hiyo, Michael Mosha na kufanyiwa kazi na tume hizo zilizoongozwa na Katibu Tawala Msaidizi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Kilimanjaro, Grace Makiluli.

Baada ya kubainika kwa tuhuma hizo, Mderu alisema baraza hilo lilimpongeza mkaguzi huyo kwa kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa kwa kuwa angeweza kudanganyika kutumia fedha hizo.

Mkuu wa Wilaya ya Hai, Gelasius Byakanwa, amepongeza baraza hilo kwa hatua hizo na kueleza kuwa kazi kubwa ya madiwani ni kusimamia mali na rasilimali za Serikali, ili wananchi wapate huduma bora za Serikali yao ya Awamu ya Tano ambayo ina dhamira ya kuwahudumia.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More