Monday, April 25, 2016

Bomba la Mafuta Kutoka Uganda kuingiza Bilioni 4.8 Kila Siku

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesema kuwa mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Hoima, Uganda hadi Tanga ukikamilika utaliingizia Taifa Sh4.8 bilioni kila siku.

Amesema fedha hizo zitatokana na usafirishaji wa mapipa 200,000 kila siku yatakayotozwa dola 12.2 (zaidi ya Sh24,000) kila moja. 

Profesa Muhongo alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuwasili nchini akitokea Kampala ambako Rais wa Uganda, Yoweri Museveni juzi alitangaza kuwa bomba hilo la mafuta ghafi kutoka Hoima, Ziwa Albert litapita katika ardhi ya Tanzania kwenda Bandari ya Tanga.

Alisema katika kujipanga kwa ajili ya mradi huo, tayari Serikali imetoa kibali kwa wanafunzi 22 ambao wamepelekwa nje ya nchi kusomea masuala ya mafuta na gesi katika ngazi ya Shahada ya Uzamili na Uzamivu. 

“Bomba litakamilika Juni 2020 na itakuwa ni zawadi kwa Rais John Magufuli kabla hajarudisha fomu ya kuomba tena kugombea awamu ya pili ya urais.Lakini tutajitahidi likamilike kabla ya muda huo,” alisema Profesa Muhongo.

Alisema utakapokamilika, yatahitajika magari 100,000 ya kutolea mizigo katika Bandari ya Tanga.

Juzi, taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa ilieleza kuwa Serikali ya Uganda imetangaza rasmi uamuzi wa kutumia Bandari ya Tanga.

Rais Museveni alitangaza uamuzi huo wakati wa mkutano wa 13 wa Ushoroba wa Kaskazini uliomalizika jijini Kampala juzi na kuhudhuriwa na Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Dk Augustine Mahiga na Profesa Muhongo.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More