Monday, October 19, 2015

UN, SMZ KUSHIRIKIANA KUKOMESHA UDHALILISHAJI WA KIJINSIA

IMG_9939

Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za Dawati la Jinsia na Watoto, Mkoa wa Kaskazini Unguja katika Kijiji cha Mahonda wakati wa ziara fupi ya kukagua miradi inayofadhiliwa na Umoja wa Mataifa visiwani humo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 70 ya Umoja huo tangu kuanzishwa.
Na Mwandishi wetu, Zanzibar.
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez amesema Umoja huo utaendelea kushirikiana na Serikali ya mapinduzi Zanzibar (SMZ) katika kukomesha vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia.
Akizungumza katika ziara ya kutembelea Dawati la jinsia la Wanawake na Watoto, Mkoa wa Kaskazini Unguja katika Kijiji cha Mahonda alisema umoja huo umelenga kusaidia uwepo wa utawala wa sheria na wenye kujali haki na utu wa binadamu kupitia mpango mkakati wake uliomo katika malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) kuanzia mwaka 2016 utakosaidia kuondoa vitendo hivyo.
Alieleza kuwa tatizo la udhalilishaji wa kijinsia sio kwa Zanzibar pekee bali ni la kidunia, hivyo umoja wa mataifa(UN) unawajibu kusaidia juhudi za serikali kupambana na tatizo hilo.
“Tushirikiane kwa kila hatua ili kuondosha vitendo hivi kwani ni tatizo na kero kwa jamii ya Zanzibar pia ni miongoni mwa ishara tosha zinazoashiria uvunjifu wa haki za binadamu.”, alisema Rodriguez na kusisitiza kuwa ili kukomesha vitendo hivyo ni kuwepo na utawala wa kisheria utakaotenda haki kwa wale wanaoozalilishwa utu wao.
IMG_9951
Aidha Bw. Rodriguez aliyataka madawati ya jinsia kutumia vyombo vya habari kuwaelimisha wananchi kupambana na vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia ili kuhakikisha vinapungua ama kuisha kabisa kwa lengo la kujenga jamii yenye uadilifu.
Naye Mtendaji wa Dawati hilo, kutoka Jeshi la Polisi Koplo, Fatma Juma alifafanua kuwa kesi za ubakaji kwa wanawake na watoto zimepungua ikilinganishwa na miaka iliyopita.
Alisema kwa sasa kuna changamoto ya utoroshwaji na utelekezaji wa watoto kesi ambazo kwa sasa ni nyingi lakini wanaendelea kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu ili kuhakikisha zinapungua.
Akizitaja changamoto zilizopo katika dawati hilo kuwa ni pamoja na kukosekana kwa ushahidi wa kina kwa baadhi ya kesi hivyo kupelekea kuharibu mwenendo mzima wa kesi kutokana na kukosekana uthibitisho.
IMG_9928
Mtendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto, Mkoa wa Kaskazini Unguja katika Kijiji cha Mahonda, kutoka Jeshi la Polisi Koplo, Fatma Juma akitoa taarifa fupi ya maendeleo ya kituo hicho tangu kufunguliwa ikiwa ni mwaka mmoja sasa kwa Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez (hayupo pichani) ikiwa ni awamu yake ya pili kutembelea Dawati hilo. Kulia ni Mtaalamu wa masuala ya ulinzi kwa watoto wa UNICEF Zanzibar, Bw. Ahmed Ali.
Alifahamisha kuwa changamoto nyingine ni jamii ya wazanzibar kuwa na tabia ya mukhari (kuoneana haya) hivyo kumaliza kesi kwa njia ya kifamilia bila ya kufuata utaratibu wa kisheria, hali inayokuwa kikwazo cha kuwafikisha katika vyombo vya kisheria wahalifu wa kesi za ubakaji.
“Bado nasisitiza ni lazima Wazanzibar tubadilike na kuondokana na masuala ya muhari kwani unawaumiza watoto wetu na tujenge utamaduni wa kujiamini kwa kutoa ushahidi ili tutokomeze janga hili.,” alisisitiza Fatma.
Pamoja na hayo alishukru msaada unaoendelea kutolewa na Umoja wa mataifa (UN) kwa kuunga mkono juhudi za serikali katika kuwawezesha katika mambo mbali mbali kwa lengo la kupunguza vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia.
Mwakilishi huyo Mkazi katika ziara hiyo alitembelea miradi mbali mbali ya umoja huo ikiwa ni moja ya sherehe za kutimiza miaka 70 ya kuanzishwa kwa umoja huo.
IMG_9935
Baadhi ya waandishi wa habari wa visiwani Zanzibar na maofisa wa Umoja wa Mataifa waliombatana na Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez (hayupo pichani) katika ziara ya kukagua miradi inayofadhiliwa na Umoja wa Mataifa visiwani humo.
IMG_9969
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akipitia kitabu cha orodha za kesi katika Dawati la Jinsia na Watoto, Mkoa wa Kaskazini Unguja katika Kijiji cha Mahonda. Kulia ni Mtendaji wa Dawati hilo, kutoka Jeshi la Polisi Koplo, Fatma Juma na kushoto ni Mtaalamu wa masuala ya ulinzi kwa watoto wa UNICEF Zanzibar, Bw. Ahmed Ali.
IMG_9963
IMG_9983
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akiwa ndani ya chumba cha dawati la Jinsia.
IMG_0009  
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akiagana na Mkuu wa Upelelezi wa Dawati la Jinsia na Watoto, Mkoa wa Kaskazini Unguja, Kombo Khamis Kombo (kulia) alipofanya ziara ya kutembelea Dawati la Jinsia na Watoto, Mkoa wa Kaskazini Unguja katika Kijiji cha Mahonda ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya sherehe za miaka 70 ya Umoja wa Mataifa tangu kuanzishwa. Kushoto ni Mtaalamu wa masuala ya ulinzi kwa watoto wa UNICEF Zanzibar, Bw. Ahmed Ali.
IMG_9904
Mradi huu ulifadhiliwa kwa pamoja kati ya Jumuiya ya Ulaya (EU) na Shirika linalohudumia watoto duniani, UNICEF.
IMG_0023
Muonekano wa jengo la Dawati la Jinsia na Watoto mkoa wa Kaskazini Unguja.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More