Friday, October 9, 2015

COSATO CHUMI AWATAKA MAFINGA MJINI WAMPUUZE WILLIAM MUNGAI NA PROPAGANDA ZAKE ZA UONGO


MGOMBEA ubunge wa jimbo la Mafinga Mjini kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Cosato Chumi amezilalamikia kampeni na propaganda alizozihita kuwa ni chafu zinazofanywa dhidi yake na mgombea wa jimbo hilo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), William Mungai.
Akizungumza na wanahabari juzi mjini Mafinga, Chumi anayepewa nafasi kubwa ya kushinda katika kinyang’anyiro hicho alisema katika mikutano yake mgombea huyo amekuwa akimtuhumu kwa wapiga kura wa jimbo hilo kwamba anao mpango wa kufuta biashara ya bodaboda  na biashara za minada katika jimbo hilo, mambo ambayo si kweli.
“Mimi Cosato Chumi, nawahakikishia kuwa makundi haya ya waendesha bodaboda, bajaji, taxi, wauza mboga, vikundi mbalimbali, wasanii, watu wa minanda na makundi yote ya wajasiriamali ni makundi muhimu sana kwangu,” alisema na kuwataka wananchi wa jimbo hilo kumpuuza mgombea huyo na propaganda zake chafu.
Alisema makundi hayo ni muhimu kwasababu ndiyo yanayorahisha upatikanaji wa huduma hizo kwa wananchi wa jimbo hilo na yanamchangomkubwa katika kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja, jimbo hilo na Taifa kwa ujumla.
“Na ndio maana katika harakati zangu za kuwakwamia vijana kutoka katika lindi la umasikini, pamoja na mambo mengi niliyofanya kwa vijana hao kabla hata sijafikiri kugombea ubunge, nilikuwa mtu wa kwanza kuja na mpango wa kuwakopesha vijana bodaboda ili wazitumie kujikwamua na umasikini,” alisema.
Alisema ili kumkosanisha na wapiga kura katika makundi hayo, mgombea mwenzake huyo amekuja na siasa za chuki, ufitinishi, uchonganishi na uongo akilenga kujinufaisha kisiasa.
Alipotafutwa kwa simu yake ya mkononi kujibu tuhuma hizo, Mungai hakupokea simu pamoja na kupigiwa mara kadhaa.
Akiomba wananchi wa jimbo hilo wamchague yeye kuwa mbunge, madiwani wote kutoka CCM na mgombea urais Dk John Magufuli, Chumi alisema: “sina sababu nyingine ya kuomba nafasi hii ya ubunge isipokuwa ni kwa ajili ya kuwatumikia kwa uadilifu, uaminifu na kwa bidii katika kuhakikisha tunainyanyua Mafinga kwa maendeleo ya kasi.
Alisema hakuna sababu kwa jimbo hilo kukosa maji, huduma za afya, umeme, barabara nzuri, wazazi kuendelea kutoa michango ya madawati wakati wamezungukwa na msitu wa taifa wa Saohill na wajasiriamali kuendesha biashara zao kwa uhuru endapo watamchagua kuwa mbunge wao.
Alisema katika taifa linaloendelea kukua na kukomaa katika siasa za vyama vingi na demokrasia ya uwazi na uwajibikaji ni muhimu wanasiasa wakajikita katika kuelezea sera, mipango na vipaumbele vya namna gani jimbo hilo la Mafinga litanyanyuliwa badala ya kupakana matope, kusingiziana na kueneza tuhuma zisizo za kweli dhidi ya wengine.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More