Saturday, February 3, 2018

MIRADI YA JAMII YA GGM UMIZA KICHWA MKOANI GEITA

Mkuu wa mkoa wa Geita,Mhandisi Robert Luhumbi akiwa ameongozana na baadhi ya wakuu wa idara wa halmashauri ya mji wa Geita pamoja na viongozi wa chama cha mapinduzi (CCM) na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa na wilaya ya Geita kwenye mradi wa vijana na wanawake uliopo magogo .

Mkuu wa mkoa wa Geita,Mhandisi Robert Luhumbi akipokewa na katibu tawala wa wilaya ya Geita,Thomas Dimme wakati alipowasili kwenye mradi wa vijana na wanawake wa magogo.

Mkuu wa mkoa wa Geita,Mhandisi Robert Luhumbi ,akipokea taarifa ya uchunguzi ambao umefanyika juu ya mradi wa vijana na wanawake   kutoka kwa mkurugenzi wa halmashauri ya mji wa Geita,Mhandisi Modest Aporinaly.
Mkuu wa mkoa wa Geita,Mhandisi Robert Luhumbi  akikagua baadhi ya vifaa ambavyo vilikuwa kwenye sehemu ya chakula(Kantine).

Mkuu wa mkoa wa Geita,Mhandisi Robert Luhumbi ,akiwa kwenye kalakana ya uchomeleaji wakati alipofika kujionea vifaa vilivyopo kwenye mradi huo.

Mkuu wa mkoa wa Geita,Mhandisi Robert Luhumbi  akipokea maelezo ya mashine ya kuchomelea kutoka kwa mmoja kati ya wahusika kwenye kamati ya uchunguzi.

Mkuu wa mkoa wa Geita,Mhandisi Robert Luhumbi  akikagua mashine ya kufyatulia matofali ya kisasa.

Na,Joel Maduka,Geita


Serikali Mkoani Geita imeeleza kusikitishwa na uendeshwaji wa miradi ya mgodi wa dhahabu wa Geita, (GGM) kwa kutozingatia sheria ya ushirikishaji kwa Halmashauri zilizopo mkoani humo na kushindwa kujulikana kwa gharama za miradi ya jamii inayotekelezwa na mgodi huo.

Hatua hiyo imekuja ikiwa ni siku  chache baada ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM)  kukabidhi mradi wa Maendeleo ya uchumi kwa Vijana na Wanawake ulipo Mtaa wa Magogo Kata ya Bombambili Halmashauri ya Mji wa Geita.

Hali hiyo ilimlazimu Mkuu wa mkoa wa Geita ,Mhandisi Robert Luhumbi  kuzulu  kwenye mradi wa vijana na wanawake uliopo kata ya Bomba mbili ,mtaa wa magogo kwa lengo la kujiridhisha baadhi ya vifaa ambavyo vilitakiwa kuwepo kwenye mradi huo na hata hivyo amebaini kuwepo kwa udanganyifu mkubwa kwenye  vifaa ambavyo  vilitakiwa kuwepo kwenye mradi huo.

Luhumbi  alisema  baadhi ya watumishi kutoka serikalini  na baadhi yao kutoka GGM wameendelea kushirikiana  kwa pamoja  kuhujumu miradi mingi  ambayo imekuwa ikilenga kuleta chachu ya maendeleo kwa wakazi wa Geita ambao wamezungukwa na Mgodi huo na kufuatia hatua hiyo ameagiza uchunguzi wa kina ufanyike ili kuwabaini wale wote ambao wameshiriki kuchakachua fedha za miradi hiyo.

“Sasa katika miradi yote ishirini na sita (26) ambayo imekwenda yote ina matatizo  na ajabu mwaka huu niliambiwa kuna fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya CSR ya mwaka huu nilikagua baadhi ya  miradi kuna mradi  mmoja nilikuta ni wa bilioni moja nukta sita lakini mimi siwezi kuficha hata tukitumia fedha vibaya kidogo tunaweza kutumia milioni mia tatu (300)  lakini bilioni moja nukta tatu inapotea  na watu kutoka ofisi zetu walikwenda mgodini wakaa na kuweka mkataba  wakurugenzi hawakuwepo mkuu wa wilaya afahamu baadae tunaambiwa fedha ipo tayari kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo nimesema sisi kama mkoa hatubariki miradi hiyo  kabisa”Alisema Luhumbi.

Hata hivyo kutokana na kuonekana upungufu kwenye miradi ya jamii Mhandisi Luhumbi amewakataa maafisa mahusiano ya jamii wa mgodi wa GGM kutokana na kushindwa kufanya shughuli  zao kwa weledi kwenye maeneo waliyopangiwa na mgodi  huo.

Na pia ameviagiza vyombo vyote vya sheria kuhakikisha wanaingia kwa undani zaidi na kufanya uchunguzi wa kutosha na ndani ya wiki moja endapo kuna mtumishi wa serikali  atakayebainika kuhujumu basi sheria ichukuliwe dhidi yake ikiwa ni pamoja na kumwajibisha.

Afisa sheria wa Mkoa huo Bi Sarah Mwangole alisema mradi wa Magogo ambao umekabidhiwa hivi karibuni umefanyika bila ya makubaliano baina ya Halmashauri na mgodi wa GGM hivyo pia wameshauri vyombo vya sheria kuingilia na kufanya uchunguzi na kwamba hadi sasa ofisini kwao hawajapata nyaraka zozote za mradi huo licha ya kuzihitaji.

Mtandao huu  umezungumza na Msimamizi wa kitengo cha mahusiano kwenye mgodi wa GGM Bw Joseph Mangilima ambaye alisema mengi  ya mambo yaliyozungumziwa hawezi kuyazungumzia yeye kwa kuwa hayahusiani na kitengo chake moja kwa moja na kwamba kazi iliyompeleka kwenye mradi huo ni kupeleka funguo za majengo baada ya kusikia mkuu wa mkoa anautembelea mradi huo.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More