Thursday, March 3, 2016

Watumishi 3 Ghala la Chakula Arusha Wasimamishwa kazi

Watumishi  watatu wa Ghala la Taifa la Hifadhi Chakula wamesimamishwa kazi, wakidaiwa kuchanganya kwa makusudi mahindi mabovu na mazuri na kuwapelekea wananchi.

Uamuzi huo ulichukuliwa mjini Arushajana na Naibu Waziri wa Mifugo, Kilimo na Ushirika, William Ole Nasha baada ya kufanya ziara kwenye ghala mkoani hapa.

Waliosimamishwa kazi kupisha uchunguzi ni Meneja Brightone Mollel ambaye ni msimamizi mkuu wa ghala na maofisa wawili kutoka Makao Makuu Dar es Salaam ambao ni Dunia Mlokozi na Silvano Mwakinyela.

Wanatuhumiwa pia kuuza mahindi hayo ya serikali kwa wafanyabiashara mbalimbali mkoani Arusha na nje ya nchi. 

Imedaiwa kutokana na vitendo hivyo, wamejinufaisha na kuwa mamilionea huku wananchi wakinyanyasika kwa kula chakula kibovu.

Hata hivyo, Meneja huyo, Mollel alimweleza waziri kuwa tuhuma zinazoelekezwa kwake si za kweli, kwani hajawahi kufanya unyama huo wala kuuza mahindi ya serikali.

Akifafanua kwa waandishi wa habari baada ya kufanya ziara ya ghafla katika ghala hilo, Naibu Waziri Nasha alisema hujuma ya kuwalisha watanzania chakula kibovu, imefanyika kwa miaka mingi na amekuwa akipata malalamiko mengi mkoani Arusha na nje ya mkoa.

Nasha alisema serikali haiwezi kuwaachia kirahisi watumishi wa aina hiyo wenye uchu wa utajiri kwa kuwaangamiza wananchi kwa maslahi yao. Alikielezea kitendo hicho kuwa si cha huruma.

Kwa mujibu wa naibu waziri huyo, mahindi mabovu ambayo yametengwa, huchanganywa na mahindi mazuri na kusambazwa kwa ajili ya matumizi ya binadamu huku wahusika wakijua wazi kuwa hayafai kwa matumizi hayo.

‘’Angalia ubovu wa mahindi haya, lakini vigogo wa ghala hili wakishirikiana na wafanyabiashara, wanachanganya na mahindi mazima na kisha wanapeleka wilayani kwenye uhaba wa chakula. 

"Wananchi wamekuwa wakilalamika kila mara kuwa mahindi yanayopelekwa huko hayafai kuliwa na hata na mbuzi au ng’ombe hawali, hali iliyonifanya kufuatilia kwa karibu na kuja kujionea mwenyewe bila kuambiwa,’’ alisena Nasha.

"Hawa watu nimewasimamisha kazi kuanzia leo (jana) mpaka uchunguzi upite ni kwa nini wanafanya hivyo, hii haikubaliki,’’ alisema Nasha.

Baadhi ya wafanyakazi wa ghala hilo na wabeba mizigo, walikiri kwamba hali ya kuchanganya mahindi mabovu na mazuri iko katika ghala hilo kwa muda mrefu na wamekuwa wakilazimishwa kufanya hivyo kwa maslahi ya baadhi ya watumishi.

Mmoja wa wafanyakazi hao, aliyeomba jina lake lihifadhiwe, alisema watendaji hao wakuu wa ghala, wana utajiri mkubwa unaohusishwa na hujuma hiyo ya mahindi.

“Kuna kigogo mmoja alimpa mtoto wake wa kike zawadi ya gari V8 VX yenye thamani ya zaidi ya Shmilioni themanini siku yake ya kuzaliwa. Baadhi ya watumishi wa serikali katika ghala hili wanaishi kama wapo peponi kwa kuwapa watanzania chakula kibovu.

"Mahindi ya serikali huuzwa na mengine kusafirishwa nchi jirani ya Kenya bila ya kubughudhiwa,” alisema mfanyakazi huyo. Mfanyakazi mwingine alisema kuna mtandao mkubwa wa kuuza mahindi ya serikali.

"Kibaya zaidi watanzania wanalishwa chakula kibovu chenye hatari kwa afya huku wao wakijitajirisha kwa mahindi mazuri yanayoenda nje ya nchi kwa njia za panya," alisema mfanyakazi mwingine aliyeomba jina lihifadhiwe.

Alisema, "Naomba Waziri unilinde kwani ninaweza kuuawa, hata nikifukuzwa kazi sioni tatizo, lakini roho inauma sana ninapoambiwa nichanganye mahindi mabovu yenye sumu na mahindi mazuri ili yakaliwe na watanzania, hiyo ilituuma sana wabeba mizigo wote’’.

Alisema malalamiko hayo waliyafikisha ofisi ya mkuu wa wilaya siku nyingi kuelezea hujuma hiyo. Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Fadhili Nkurlu alikiri kuwa na taarifa hiyo na alisema ndio maana amekuja na waziri husika, anayeshughulika na sekta hiyo.

Nkurlu alisema pia Waziri mwenyewe amekiri kupata malalamiko katika wilaya za Karatu, Ngorongoro na Simanjiro kuwa mahindi ya misaada yanayopelekwa huko, hayafai kuliwa na binadamu kwani hata mifugo inakataa kula.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More