Thursday, March 3, 2016

Binti wa Raila Odinga Aomba Radhi Watanzania kwa kauli yake kwamba Olduvai Gorge iko nchini Kenya

Mtoto wa Waziri Mkuu wa zamani wa Kenya, Raila Odinga, Rosemary amewaomba radhi Watanzania kwa kauli yake kwamba Olduvai Gorge iko nchini humo.

Rosemary alisema hakuwa na nia mbaya alipotoa kauli hiyo, bali aliitoa kwa bahati mbaya akimaanisha eneo jingine lililoko Kenya linaloitwa Olorgesalile.

Alifafanua kuwa matamshi hayo hayakulenga kupotosha ukweli, bali ulimi uliteleza.

Katika maelezo aliyotoa kupitia akaunti yake ya Facebook, Rosemary aliandika:

“Habari za jioni. Nimekuwa nikikumbushwa kuhusu tukio lililotokea wakati nahudhuria kongamano la vijana New York, miezi saba iliyopita.

Niliteleza ulimi kwani sikumaanisha Olduvai Gorge badala yake nilitaka kumaanisha Olorgesalile,” alisema na kuongeza:

“Nawapa pole Watanzania kutokana na usumbufu uliojitokeza, kaka zangu na dada zangu poleni sana na Olduvai Gorge yenu bado iko salama.”

Binti huyo alihitimisha kwa kuweka hotuba yake aliyoitoa kwenye kongamano hilo akisema ililenga kuleta umoja na mshikamano.

Tangu kutolewa kwa kauli hiyo, kumekuwa na mlolongo wa shutuma zinazoelekezwa kwa binti huyo wa Odinga huku baadhi ya Watanzania wakisaini azimio maalumu kumtaka ombe radhi ambalo waliosaini wamefikia 17,000.

Tangu wiki iliyopita, kumekuwapo na mkanda wa video unaosambaa kwenye mitandao ya kijamii ikimuonyesha Rosemary akihutubia mkutano jijini New York huku akidai Bonde hilo lililogunduliwa mtu wa kale la Olduvai Gorge linapatikana nchini Kenya.

Mapema, Serikali ya Tanzania imesema itachukua hatua za kidiplomasia endapo ungepatikana uhakika juu ya taarifa zinazoenezwa na mitandao ya kijamii kuwa raia wa Kenya huzitaja baadhi ya tunu za Tanzania kuwa zinamilikiwa na nchi yao.

Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo), Assah Mwambeni alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari jana akisema Serikali inafanya uchunguzi juu ya taarifa hizo.

Hata hivyo, alisema hali hiyo inaonyesha ni jinsi gani nchi Tanzania inazidi kuwa maarufu kwa mazuri yake mpaka majirani wanatamani miliki zake.

Mwambene alikuwa anazungumzia taarifa za mitandao zilizowahusisha raia wa Kenya kutamba kuwa Mlima Kilimanjaro, Olduvai Gorge na Mbuga ya Serengeti vipo nchini Kenya na ripoti za hivi karibuni kuwa mwanasoka wa kimataifa, Mbwana Samatta na mwanamuziki Diamond Platinumz ni raia wa Kenya.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More