Friday, March 17, 2017

ALIYEKUWA MWENYEKITI WA CCM MKOA WA IRINGA ANENA, NI BAADA YA UANACHAMA WAKE KUFUTWA





ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa, Dk Jesca Msambatavangu amesema baada ya kufukuzwa uanachama wa chama hicho, hatma yake kisiasa inategemea majibu atakayopewa na Mwenyezi Mungu.

Akizungumza HabariLeo nyumbani kwake mjini Iringa jana, Dk Msambatavangu alisema; “Mungu niye atakeyenionyesha njia siwezi kuwa na majibu ya haraka, kilichonikuta hakina tofauti na kufiwa.”

Mbali na kufananisha tukio lililomkuta na msibwa, alisema maamuzi ya kufukuzwa uanachama yaliyofanywa na Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM hakuyapokea kwa mshutuko mkubwa kwasababu alisikia taarifa hizo zikisemwasemwa kabla ya kikao hicho.

Pamoja na kwamba hajui tuhuma iliyomfukuzisha uanachama kwakuwa bado hajapewa rasmi barua ya kufukuzwa uanachama huo, alisema taratibu zilizofikia maamuzi hayo zilifuatwa.

“Kwahiyo nikipewa barua rasmi ya kufukuzwa uanachama nadhani nitakuwa na lakuongea kwasababu ndani ya barua hiyo kutakuwa na sababu iliyopelekea maamuzi hayo dhidi yangu,” alisema.

Alisema ameanza na atajitahidi kwa kadri ya uwezo wake na kwa mapenzi ya Mwenyenzi Mungu kuishi nje ya mfumo wa CCCM alioupenda toka moyoni mwake na ambao alikuwa tayari kupoteza maisha yake kwa ajili yake.

Akiwa mwana CCM wa kufana na kupona, Dk Msambatavangu alisema alitumia akili, utaalamu na nguvu zake zote, na rasilimali vitu na fedha kuhakikisha chama hicho kinaimarika na kuaminika kwa watanzania.

“Wananchi wa mkoa wa Iringa ni mashahidi wazuri kwangu, kazi niliyoifanya nikiwa ndani ya chama hicho ilikuwa kubwa na kuna wakati ilitaka kuhatarisha maisha yangu,” alisema na kutoa mfano wa jinsi alivyonusurika wakati wa Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Kalenga, mwaka 2013.

Alisema huenda yote mazuri na makubwa aliyoyafanya akiwa ndani ya chama hicho yakasahaurika na akaomba wenye mapenzi mema juu yake, wamuombee avuke salama jaribio alilopitia.

“Sisi wakristo tunaamini kila jibu lina mtihani wake. Huu ni mtihani wangu, Mungu ameruhusu nipite njia hii na yeye ndiye atakayekuwa wa mwisho kutoa hukumu sahihi juu ya hili kwasababu sikuwahi kufikiria kama kuna siku nitafukuzwa uanachama,” alisema.

Akiwatia moyo wanaCCM wanaobaki ndani ya chama hicho alisema; “askari mmoja akifa vitani, ni wajibu wengine wakachukua silaha yake na kuendeleza vita hiyo.”

Kuhusu Edward Lowassa
Dk Msambatavangu alisema kabla ya mchakato wa kumpata mgombea urais wa CCM mwaka 2015, yeye na wanaCCM wengine wengi walimuunga mkono Waziri Mkuu aliyajiudhuru, Edward Lowassa.

“Tulimuunga mkono tukijua hiyo haikuwa dhambi kwakuwa ni mwanaCCM mwenzetu na tuliamini angeweza kupokea kijiti toka kwa Dk Jakaya Kikwete na kusukuma gurudumu la maendeleo ya Taifa mbele zaidi,” alisema.

Alisema kama ambavyo wao waliamua kumuunga mkono Lowassa, wapo wana CCM wengine waliwaunga mkono wagombea wengine, na kwa mujibu wa taratibu za chama hicho na ndio sababu wengi walijitokeza kugombea nafasi hiyo.

Alisema baada ya CCM kukamilisha mchakato wa kumpata mgombea wao, walikuwepo waliohama  chama hicho lakini yeye na wanaCCM wengine wengi waliokuwa wanamuunga mkono Lowassa walibaki na kukisaidia chama kupata ushindi kwasababu huo ndio wajibu wao.

“Na mimi nilibaki kwasababu CCM ilikuwa kwenye damu yangu, sio mpitaji lakini lazima nikubaliane na hali halisi damu hiyo itakwisha kwasababu si mwana CCM tena,” alisema.

Maisha yake nje ya siasa
Kuhusumaisha yake nje ya siasa, Dk Msambatavangu alisema ataelekeza nguvu zake kuimarisha shughuli zake za ujasiriamali.

“Nguvu yangu kubwa sasa itakuwa huko na kwenye shughuli za kilimo na ufugaji. Nataka nilime sana na nifuge sana mifugo aina mbalimbali jamii ya ndege, lakini na sungura pia.”

Kuhusu michango yake kwa jamii, alisema ataendelea kujitolea kusaidia shughuli mbalimali za kijamii kama alivyokuwa akifanya wakati akiwa mwanachama na kiongozi wa CCM.

“Na wale watakaotaka kuonana na mimi, kwasasa tutakutana makanisani, nadhani huko nitakuwa naonekana sana wakati huu nikiendelea kupata uzoefu wa kuishi nje ya siasa za CCM,” alisema.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More