Tuesday, May 10, 2016

Waziri Ataka Wakurugenzi NHC Washindanishwe

NAIBU  Waziri  wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo  ya Makazi, Angeline Mabula, ametaka wakurugenzi  wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) katika mikoa yote washindanishwe   kujua utendaji kazi wao.

Waziri Mabula, alitoa kauli hiyo Dar es Salaam mwishoni mwa wiki  wakati akifungua  kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi  wa shirika hilo kilichokuwa kikijadili mipango na makisio  ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka 2016/17 kabla ya kuwasilishwa bungeni.

Alisema  hatua hiyo itasaidia kutambua wakurugenzi ambao wanasubiri kubebwa na wenzao kwa kushindwa kufanya kazi kwa weledi.

Alisema ujenzi na ununuzi wa nyumba unahitaji fedha nyingi, wananchi hununua nyumba kupitia mikopo kutoka benki.

"Serikali inatambua umuhimu wa taasisi za fedha  katika kusaidia ukuaji  wa sekta ya nyumba jambo ambalo hufanywa duniani kote, "alisema.

Alisema Serikali inatambua bado kuna changamoto  ya riba kubwa ya mikopo  ya nyumba  inayotozwa  na benki ambayo sasa ni kati ya asilimia 18 hadi 25.

Alisema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwamo Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ili kuona namna bora ya kuwezesha benki kupunguza riba katika mikopo ya nyumba.

“Serikali itahakikisha benki zote  zinashiriki  kukopesha wananchi   waweze kununua nyumba, kufanya hivi kutachochea ukuaji wa uchumi na wananchi watatumia nyumba zao kupata mikopo ya benki kwa ajili ya kuanzisha miradi yao ya maendeleo."

Mkurugenzi Mkuu  NHC, Nehemia Mchechu, alisema   moja ya majukumu  ya baraza  hilo ni kujadili mipango  na makisio ya mapato  na matumizi ya wizara  kabla ya kuwasilishwa bungeni.

“Serikali imeweka msisitizo  zaidi katika ukusanyaji wa mapato, kupitia kikao hiki tutapata  maoni  na mikakati  ya kuboresha  ukusanyaji wa kodi za ardhi,” alisema.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More