Monday, May 9, 2016

Aswekwa Mahabusu Kwa Kusema Uongo Mbele ya Mkuu wa Mkoa

Mkazi wa Kijiji cha Natambiso, Kata ya Natta wilayani Serengeti Mkoa wa Mara, Christopher Nyamasagi ameswekwa mahabusu kwa tuhuma za kutoa taarifa ya uongo kuwa mjumbe mmoja mwanamke aliombwa rushwa ya ngono ili wapate mikopo ya Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF).

Alitoa madai hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika Shule ya Msingi Natta Mbisso mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, Magesa Mulongo.

Kabla ya kukamatwa, Nyamasagi aliyekuwa na bahasha ya kero mkononi, alidai kuwa walichanga fedha ili waanzishe Saccos ya kukopeshwa fedha na NSSF Mkoa wa Mara.

“Mkuu wa Mkoa tulikamilisha vigezo vya usajili, baada ya kuchangia zaidi ya Sh11 milioni, wakatoa elimu namna ya uendeshaji na baadaye tukafungua akaunti mwaka 2014, tukaanza kufuatilia mikopo, tulisumbuliwa sana na kufikia hatua ya kutuambia kama tunataka mkopo, mjumbe mmoja mwanamke atoe rushwa ya ngono ili tupatiwe,” alidai Nyamasagi.

Wakati mkuu huyo wa mkoa akishangazwa na madai hayo, alisimama mwanamke mmoja wa kijiji hicho na kukanusha huku akitaka Nyamasagi awaombe radhi wanawake kwa taarifa yake ya uongo inayolenga kuwadhalilisha.

Ndipo Mulongo alimuagiza kamanda wa polisi wilayani hapo amkamate Nyamasagi na kumuweka mahabusu kwa tuhuma za kudanganya. Alisema kikao hicho kililenga kujadili kero na siyo kudhalilishana.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More