Wednesday, May 25, 2016

MBUNGE WA MAFINGA MJINI ATOA MSAADA WA AMBULANCE JIMBONI KWAKE

MBUNGE wa Mafinga Mjini, Cosato Chumi akizindua
gari la kubeba wagonjwa (ambulance) 
 na fredy mgunda,iringa
MBUNGE wa Mafinga Mjini, Cosato Chumi kwa kushirikiana na asasi ya kimataifa ya Rafiki Surgical Mission ya Australia ametoa msaada wa gari la kubeba wagonjwa (ambulance) kwa ajili ya matumizi ya hospitali ya wilaya ya Mufindi, mkoani Iringa iliyopo katika jimbo lake hilo.

Gari hilo aina ya Toyota Hiace lenye thamani ya Sh Milioni 40 lilikabidhiwa jana kwa uongozi wa halmashauri ya mji wa Mafinga inayosimamia uendeshaji wa hospitali hiyo katika mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa mashujaa, mjini Mafinga.

Akikabidhi msaada huo Chumi alisema; “napenda ifahamike kwamba gari hilo limenunuliwa na asasi hiyo ambayo mimi ni rafiki yao mkubwa. Uadilifu na uaminifu kwa taasisi hiyo umetufanya tushirikiane vyema katika mambo mengi kwa faida ya wananchi wa jimbo langu la Mafinga.”

Alisema  gari hilo la wagonjwa ni rafiki kwa wagonjwa na wajawazito kwa kuwa lina vifaa tiba vinavyoweza kutumika kutolea huduma wakati wakipelekwa hospitalini.

Baada ya kukabidhi gari hilo, Chumi ambaye ni mbunge wa kwanza wa jimbo hilo jipya, mkoani Iringa alikumbusha vipaumbele vyake kwa wapiga kura wake kuwa ni kuhakikisha linapata huduma bora ya maji, elimu, afya na miundombinu ya barabara.
Akishukuru kwa msaada huo, Kaimu Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga, Dk Innocent Mhagama alisema kabla ya msaada huo, hospitali hiyo ya wilaya ilikuwa na gari moja tu la kubeba wagonjwa.

“Pamoja na kuhudumia hospitali hiyo ya wilaya, gari hilo moja lilikuwa likihudumia vituo vingine 18 vya kutolea huduma katika wilaya hiyo hivyo,” alisema.

Alisema kupatikana kwa gari hilo jipya kutasaidia kuboresha huduma hiyo  kwa kuokoa maisha ya wagonjwa na maisha ya mama na mtoto ambayo ni kipaumbele katika utoaji wa huduma za afya.

Akizungumzia huduma ya mama na mtoto katika hospitali hiyo ya wilaya, Dk Mhagama alisema kwa wastani wajawazito 500 wanajifunga kila mwezi hospitalini hapo.

“Kati yao wajawazito zaidi ya 100 huwa wanapata huduma za dharula huku wastani wa wajawazito 10 wakipatiwa huduma za rufaa,” alisema.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga, Charles Makoga alisema halmashauri yake kwa kushirikiana na mbunge huyo itahakikisha inatekeleza ahadi mbalimbali zilizotolewa na Chama cha Mapinduzi (CCM), Rais Dk John Magufuli, mbunge na madiwani ili kuboresha huduma kwa watu wake.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More