Saturday, April 29, 2017

DK MSAMBATAVANGU AENDELEA KUSHIKILIWA NA POLISI

Tokeo la picha la jesca msambatavangu
Jeshi la Polisi Mkoani Iringa linaendelea kumshikilia Mwenyekiti wa zamani wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Iringa, Dk Jesca Msambatavangu anayetuhumiwa kumshambulia na kumsababishia maumivu makali mwilini mwanamke mmoja, ambaye jina lake bado halijafahamika.

Mpaka jana jioni wakili wake aliyetajwa kwa jina moja la Chaula na wadhamini wake walikuwa wakiendelea na taratibu za kumdhamini kada huyo wa CCM wa zamani huku kukiwa hakunataarifa zozote zinazoashiria kupewa dhamana hiyo.

Akizungumza kwa kifupi kuhusiana na tukio hilo juzi, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Julius Mjengi alisema kada huyo wa zamani wa CCM alikamatwa juzi mchana, akituhumiwa kutenda kosa hilo wiki iliyopita akiwa na wenzake ambao majina yao yamehifadhiwa kwakuwa wanaendelea kutafutwa.

RPC Mjengi alisema Msambatavangu na wenzake wanadaiwa kumshambulia mwanamke mmoja mkazi wa Kibwabwa (hakutajwa jina kwasababu za kiupelelezi) na kisha kumchoma sindano takoni ambayo mwanamke huyo hajui ni ya kitu gani.

Msambatavangu alikuwa miongoni mwa vigogo wa CCM ‘waliotumbuliwa’ hivi karibuni na kufukuzwa uanachama katika Mkutano Maalum wa CCM uliofanyika Machi, mwaka huu.

Baadhi ya marafiki na ndugu wa jirani wa Dk Msambatavangu jana walikusanyika nje ya ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa katika kile kilichoonekana kutaka kujua hatma ya mwanasiasa huyo ambaye pia ni mfanyabishara maarufu mjini Iringa.

Kabla ya kutoa amri iliyowataka watu hao kutawanyika katika eneo hilo kwa kile kilichoelezwa walikuwa katika mkusanyiko usio halali, Jeshi la Polisi liliwazuia watu hao kuingia ndani ya uzio wa ofisi hiyo ya RPC.

Baadhi ya waandishi wa habari waliofika katika ofisi hizo nao hawakupata fursa ya kuingia ndani ya uzio wa ofisi hizo ili kukutana na RPC kwa lengo la kupataa taarifa kamili ya kukamatwa kwa mwanasiasa huyo.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More