Friday, February 19, 2016

Askari Hifadhi ya Kinapa Watuhumiwa Kuwadhalilisha Wanawake kwa Kuwapiga, Kuwabaka

Serikali mkoani Kilimanjaro imeuagiza uongozi wa Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (Kinapa), kuwachukulia hatua askari wanaodaiwa kuwanyanyasa wanawake wanaoingia katika Misitu ya Nusu Maili kukata nyasi na kuokota kuni.

Mkuu wa mkoa huo, Amos Makala alitoa agizo hilo jana kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Mshiri wilayani hapa.

Alisema katika ziara aliyofanya kwenye vijiji vinavyozunguka msitu huo, wanawake wamekuwa wakilalamika kufanyiwa vitendo vya ukatili, ikiwamo ubakaji na kupigwa wanapokutwa na askari hao wakikata nyasi kwa ajili kulisha ng’ombe na kuokota kuni za kupikia.

“Kinapa najua wapo baadhi ya askari wenu ambao siyo waaminifu, wamekuwa wakiwafanyia vitendo vya kikatili na vya kinyama wanawake wanaoingia katika Msitu wa Nusu Maili. Kwa hiyo nawaagiza kuwachukulia hatua za kisheria mara moja,” alisema Makala Mkuu huyo wa mkoa alisema vitendo hivyo ni vya aibu na vya kusikitisha kwa taasisi kubwa ya umma.

“Mtu mzima hawezi kusimama kwenye hadhara ya watu wengi namna hii na kusema uongo katika mambo makubwa kama kubakwa na kutembezwa kwenye hifadhi siku nzima, kupigwa na kukalishwa kwenye siafu,” alisema Makalla.

Mmoja wa wakazi wa kijiji hicho, Veronica Mlay alisema wamekuwa wakiingia katika hifadhi hiyo siku za Jumatano na Jumamosi ambazo wameruhusiwa kukata nyasi na kuokota kuni, lakini baadhi ya askari wa Kinapa wanapowakuta huwafanyia vitendo vya unyanyasaji.

Kaimu mhifadhi wa hifadhi hiyo, Charles Ngendo alisema vitendo hivyo viliwahi kulalamikiwa miaka ya nyuma katika ofisi yake na kuvishughulikia.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More