Tuesday, May 29, 2018

JUMIA FOOD YASHIRIKIANA NA WATEJA KUSAIDIA WATOTO


Na Jumia Food Tanzania

Katika kipindi hiki cha mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani, Jumia Food kwa kushirikiana na wateja wake inaendesha kampeni ya kusaidia kituo cha kulelea watoto yatima cha Maunga kilichopo Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Kampuni hiyo inayojihusisha na huduma ya chakula kutoka migahawa mbalimbali jijini Dar es Salaam kwa njia ya mtandao, imeona ni vema kuwashirikisha wateja wake kwani wao ndio wadau wake wakubwa.

Kampeni hiyo inayokwenda kwa jina la ‘STANDY BY ME,’ kwa kiasi kikubwa inawategemea wateja kwa sababu kwa kila huduma ya chakula watayoifanya kupitia mtandao wa Jumia Food itakwenda moja kwa moja kumsaidia mtoto mmoja kituoni hapo.


Akifafanua namna wateja wanavyoweza kuchangia, Meneja Uhusiano wa Umma wa Jumia Food Tanzania, Kijanga Geofrey, amesema kuwa, “ni rahisi kushiriki kwenye kampeni hii kwani hatua za kufuata ni zilezile za kawaida anazozifanya mteja anapoagiza chakula. Kinachobadilika ni pale anapotaka kukamilisha huduma yake katika sehemu ya malipo itampasa atumie nenosiri 'ASANTE.’

Baada ya kuweka nenosiri hilo mteja atakuwa amejihakikishia kuchangia mtoto mmoja wa kituo cha Maunga. Kitakachofanyika kwa upande wa Jumia Food ni kuhesabu idadi ya huduma zote za kuagiza chakula zilizofanywa kwa kutumia neno ‘ASANTE.’ Idadi hiyo ndiyo itakayobainisha kuwa ni wateja wangapi wamehamasika kushiriki katika kampeni hiyo.
“Ningependa kuwatoa wasiwasi wateja wetu kwamba watapata huduma yao ya chakula kama siku zote, huku Jumia Food ikipeleka sehemu ya mchango wao kuwasaidia watoto hao. Kwa hiyo, sisi pia tutachangia kiasi fulani ambacho baada ya kukusanywa kitatumika kununulia mahitaji mbalimbali ambayo yatawasilishwa katika kituo cha Maunga. Ningependa kuchukua fursa hii kuwataka wateja wetu na watanzania kwa ujumla kujitokeza kwa wingi zaidi ili kuwawezesha watoto hawa kupata mahitaji yao ya msingi,” alihitimisha Geofrey.

Kama haujawahi kutumia huduma za Jumia Food, ni rahisi kufanya hivyo. Unaweza kuagiza huduma ya chakula kwa kuingia kwenye tovuti yao ambayo ni www.food.jumia.co.tz au kupitia App yao inayopatikana kwenye simu ya mkononi. Baada ya kuingia, jaza jina la eneo ulipo, itakuja orodha ya migahawa kadhaa iliyo karibu nawe pamoja na aina ya vyakula unavyohitaji, kamilisha huduma kwa kuhakikisha gharama ya huduma pamoja na kujaza taarifa zako binafsi ambazo zitatumika kuletewa chakula na muwakilishi kutoka Jumia Food.  

Huduma za Jumia Food zinaweza kutumiwa na mtu wa kipato chochote kwa sababu unaweza kuagiza chakula kuanzia shilingi 500 na kuletewa mpaka mlangoni kwako.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More