Thursday, June 2, 2016

Wabunge 7 wa Upinzani Waliosimamishwa Kuhudhuria Vikao vya Bunge Waongezewa Adhabu

Wabunge saba wa upinzani waliosimamishwa bungeni, watakumbana na kibano kingine cha kukatwa mshahara na posho kwa kipindi chote cha kutumikia adhabu.

Wabunge hao ambao Jumatatu walisimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge kwa muda tofauti kwa madai ya kukiuka kanuni ni Zitto Kabwe (Kigoma Mjini), Tundu Lissu (Singida Mashariki), Halima Mdee (Kawe), Ester Bulaya (Bunda Mjini), John Heche (Tarime Vijijini) na Godbless Lema (Arusha Mjini).

Adhabu hiyo ilitolewa  kama azimio la Bunge baada ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kupendekeza wabunge hao waadhibiwe kutokana na kuomba mwongozo wa kiti cha Spika kwa jambo ambalo tayari lilishatolewa uamuzi.

Habari zilizopatikana bungeni zilieleza kuwa wabunge hao watakumbana na Kanuni ya Bunge ya 75, ambayo inahusika na masharti ya mbunge aliyesimamishwa kazi.

Naibu Katibu wa Bunge (Shughuli za Bunge), John Joel alithibitisha kuwa utekelezwaji wa kanuni hiyo utafuatwa kwa wabunge wote ambao wamefukuzwa.

Akizungumzia hatua hiyo, Heche alisema hadi sasa hajapata barua ya kusimamishwa Bunge, hivyo hata kama watakata posho au mshahara haimsumbui kwa kuwa hawezi kusikitikia kitu hicho wakati haki inaminywa.

Zitto alisema hajasikia taarifa hizo za kukatwa mshahara kwa kuwa hajapewa barua inayoeleza mambo hayo wala ya kusimamishwa Bunge.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More