Saturday, May 13, 2017

MBUNGE WA MAFINGA AITAKA SERIKALI KUSITISHA ZUIO LA KULIMA VINYUNGU NA KUWEKWA X NYUMBA KWA HOJA YA UMBALI WA MITA SITINI


Mbunge wa Mafinga Mjini Cosato Chumi ameitaka Serikali kusitisha mara moja zuio la kulima vinyungu mpaka hapo tafsri ya umbali wa mita sitini kutoka vyanzo vya maji itakafafanuliwa ipasavyo. 

Akichangia wakati Bunge limekaa kama Kamati  kupitisha bajeti ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji , Chumi aliondoa shilingi na kuelezea kuwa suala la mita sitini limetafsriwa tofauti na kuzua taharuki kwa Wananchi ambao baadhi yao nyumba zao zimewekwa alama ya X.

'Mhe Naibu Spika suala la kilimo cha Vinyungu ni suala la maisha kwa Wananchi wa Mafinga, Mufindi, Kilolo, Njombe na mikoa ya Ruvuma na Morogoro, na limekuwa likifanyika miaka nenda rudi na hakujawai kutokea athari yoyote ya kimazingira"

Akiombwa kuungwa mkono na Wabunge wenzake, Chumi alisema kuwa tafsri ya mita sitini imekuwa ikitumika vibaya na kuwanyanyasa Wananchi ambao kilimo cha vinyungu ni muhimu kwa maisha yao. 

Wakichangia hoja hiyo Wabunge wa Kilolo- Venance Mwamoto, Mbunge wa Mlimba- Suzan Kiwanga, Mbunge wa Bunda -Mwita Getere, Mbunge wa Vwawa -Japhet Hasunga na wa Kinondoni -Maulid Mtulia walisema kuwa hoja ya Chumi ni ya msingi hivyo serikali isitishe mpaka hapo itakapothibitika mita sitini ni kutoka umbali gani. 

Akitilia msisitizo katika hoja hiyo Mhe Mwamoto alisema kuwa ameuliza swali hilo zaidi ya Mara tano lakini hakuna jibu la kueleweka kutoka Serializing.  'Kwanza wananchi hawajashirikishwa, pili hiyo njia mbadala mtakayowapa ni ipi " aliuliza na kuongeza kuwa ni lazima serikali iwaambie wananchi mita sitini ni kutoka wapi.

Mhe Kiwanga alishangazwa na kinacjoitwa Kamati ya Bonde la Rubada na watu wa Nemc ambao wamezua taharuki huko Kilombero kwa kuwatisha wananchi na kuwataka waondoke kisa mita sitini.

"Kule kwetu kila baada ya kilometa mbili unakutana na mto au kijito, na maeneo ya vyanzo vya maji tunayatunza eti Leo ooh mita sitini hii sio Sawa " alihoji Mbunge huyo wa Mlimba.

Akijibu hoja hiyo, Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais- Mazingira Lwaga Mpina alisema kuwa suala la mita sitini ni la kisheria hata hivyo Serikali iko tayari kwenda Mafinga ili kuona hali halisi na kufanya tathmini.

"Inawezekana  hao wanaoweka x ni watu wa halmashauri au watu wa Nemc, hata hivyo sheria kipengele cha 57 (2) kinatupa sisi nafasi ya kuangalia Hali halisi na kupunguza hizo mita sitini, nmemuelewa Mhe Chumi, tutaenda kuangalia tuone nini cha kufanya. 

Waziri wa Nchi Tamisemi George Simbachawene alifafanua kuwa ni kweli sio kila vinyungu ni chanzo cha maji hata hivyo, ni vizuri Serikali ikapewa Muda na kufanya tathmini.

"Kwa kweli ni ngumu wananchi wale kukuelewa kuwazuia kulima vinyungu,  kitu cha muhimu kama alivyoeleza Waziri wa Mazingira, serikali tupewe Muda tukatizame Hali halisi na kuona cha kufanya:

Kufuatia hoja hizo, Chumi aliitaka serikali kusitisha kwa muda mpaka hapo Naibu Waziri wa Mazingira atakapofanya ziara. 

Lakini pia alielezea masikitiko yake kuwa, pamoja na Waziri wa Maji Lwenge kukiri kuwa Iringa ni mkoa unaotegemewa kwa vyanzo vya maji, Lakini bajeti ya maji haizingatii hali hiyo na badala yake wamepewa bajeti kiduchu.

Akizungumza baadae na waandishi wa Habari, Chumi alisema kuwa amekuwa akipokea simu na meseji za malalamiko kutoka kwa wananchi wa Mafinga wakieleza kuwa wamezuiwa kulima vinyungu na baadhi yao nyumba zao zimewekwa X kwa madai kuwa ziko ndani ya mita sitini kutoka mtoni. 

"Kwa kweli suala la kutuzuia kulima vinyungu hatuwezi kukubali kwa sababu ni Sawa na kutukata mikono", aliongeza Mbunge huyo wa mafinga Mjini na kusisitiza kuwa watu wa Mafinga na mkoa wa Iringa kwa ujumla wamekuwa watunzaji wazuri wa vyanzo vya maji, iweje Leo wazuiwe kulima vinyungu, kwa madai tu ya mita sitini. 

Kilimo cha vinyungu hulimwa wakati wa kiangazi kwenye maeneo ambayo ni  ama ni mabonde au yenye kuhifadhi unyevunyevu, na kimekuwa mkombozi wa wanawake katika kunyanyua uchumi wao. 

Ninaiomba serikali isitishe suala hili ili kuondoa taharuki mpaka hapo tathimini itakapofanyika, mana Wananchi wanaolima vinyungu sio vyanzo vya maji, 
Ieleweke sio kila kwenye vinyungu ni chanzo cha maji:

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More