Friday, August 5, 2016

Mwenyekiti wa mtaa adaiwa kumpa mimba mwanafunzi

Mwenyekiti wa Mtaa wa Sangabuye, kata ya Igombe wilayani Ilemela mkoani Mwanza anayejulikana kwa jina la John Mayala anashikiliwa na polisi kwa kosa la kumtorosha na kumpa ujauzito mwanafunzi.

Mwanafunzi huyo amefahamika kwa jina la Lucy Daudi, anayesoma kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Sangabuye ambaye anakadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka 14 hadi 17.

Aidha jeshi la polisi pia linamshikilia mama mzazi wa mwanafunzi huyo aitwaye Agnes Kadilana mwenye umri wa miaka 48 mkulima, mkazi wa Sangabuye kwa kosa la kushindwa kutoa ushirikiano kwa polisi pindi alipohojiwa kuhusiana na tukio hilo.

Inadaiwa kuwa mama huyo alishiriki katika kumtorosha binti yake kwenda kuishi kinyumba na mtuhumiwa baada ya kupewa fedha.

Mama huyo amedai kuwa binti yake aliamua mwenyewe kuacha shule kwa madai kuwa shule imemshinda. "Yeye mwenyewe alisema hawezi kusoma, akasema ajifunze cherehani, sasa sijui" Amesema mama huyo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza DCP Ahmed Msangi ametoa wito kwa wakazi wa mkoa huo hususani wanaume wenye tabia ya kuwa na mahusiano ya kimapenzi na wanafunzi pamoja na wasichana wenye umri chini ya miaka 18 kuacha mara moja kwani ni kinyume cha sheria bila kujali kama palikuwa na makubaliano au la.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More