Tuesday, August 30, 2016

DC STAKI AWATAKA WANANCHI KUACHANA NA KILIMO CHA MIRUNGI

Mkuu wa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro Mhe Rosemary Staki akizungumza na wananchi katika moja ya mikutano ya kazi 
Mkuu wa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro Mhe Rosemary Staki akishiriki uchimbaji wa Barabara
 Wananchi kazini
 Barabara imeanza kukamilika
Mwonekano wa wananchi wakishirikiana na Mkuu wa wilaya ya same katika uchimbaji wa barabara
Wananchi wakiwa makini kumsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro Mhe Rosemary Staki mara baada ya kushiriki shughuli za maendeleo
Na Mathias Canal, Kilimanjaro

Wananchi Mkoani Kilimanjaro wametakiwa kuachana na kilimo cha bangi pamoja na mirungi kwani vinaathiri asilimia kubwa ya Vijana ambao ni nguvu Kazi ya Taifa.

Hayo yemebainishwa na Mkuu wa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro Mhe Rosemary Staki wakati akizungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Chome Wilayani humo.

Dc Staki amesema Mirungi na bangi vinaathiri zaidi nguvu kazi ya Taifa kutokana na Vijana wengi wanapotumia hujihusisha na mambo ovu ikiwemo wizi na ujambazi, Ngono zembe, kushinda vijiweni pasina kufanya Kazi pamoja na matendo ya unyanyapaa ikiwemo ubakaji.

Sambamba na hayo pia Mkuu huyo wa Wilaya ya Same alishirikiana na wananchi katika shughuli za maendeleo kabla ya mkutano huo ambapo alishiriki katika shughuli za ukarabati wa Barabara ya Bangala-Chome iliyopo Kijijini Gwang'a na Barabara ya Shengena iliyopo katika Kijiji cha Mhero.

Staki ameshiriki zoezi hilo ikiwa ni muendelezo wa kuhamasisha wanachi kuendelea kupenda kufanya Kazi za maendeleo na kuwatia Moyo ili watambue kuwa uongozi wa Wilaya utashirikiana vyema na unaunga mkono juhudi za utendaji wa wananchi.

Baadhi ya wananchi wamempongeza Mkuu huyo wa Wilaya kwa namna ambavyo anajituma na kushirikiana nao katika shughuli za maendeleo ambapo wamemuomba kuendelea kufanya hivyo ili kuamsha ari ya utendaji na ikiwezekana awachukulie hatua za kinidhamu wananchi ambao wanarudisha nyuma shughuli za maendeleo.

Katika hatua nyingine Dc Staki amewataka wananchi kujiunga na mfuko wa Bima ya Afya (CHF) ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za kiafya pindi wanapougua na kuondokana na kadhia ya kuchelewa kuapatiwa huduma.

Pia aliwasihi Vijana, kina mama na kina baba kuanzisha vikundi vya Ujasiriamali ili kupatiwa mikopo na serikali na kuondoa dhana ya kutoshirikishwa na kuilaumu serikali kwa kila jambo.

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More