Thursday, March 14, 2024

ADEM YAWAPIGA MSASA WALIMU WAKUU 4,620 WA MIKOA 6 TANZANIA BARA

Katibu Tawala Wilaya ya Nachingwea Mbarouk Balozi amefunga mafunzo  ya uongozi, usimamizi na uendeshaji wa shule za msingi yaliyoendeshwa kwa Walimu Wakuu wa Shule za Msingi za Mikoa wa Simiyu, Kigoma, Tanga, Kilimanjaro, Mbeya na Mtwara chini ya mradi wa BOOST na kusimamiwa na Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM)
Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Elekezi -ADEM Dkt. Alphonce Amuli ameeleza kuwa hadi sasa ADEM imeshatoa mafunzo kwa walimu wakuu 4,522 katika awamu ya kwanza ya mafunzo hayo, na katika awamu hii mafunzo hayo yametolewa kwa Walimu Wakuu 4,620 katika Mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Simiyu, Mbeya, Kigoma na Mtwara
Baadhi ya walimu wakuu walioshiriki mafunzo hayo



Na Fredy Mgunda,Lindi

Katibu Tawala Wilaya ya Nachingwea Mbarouk Balozi amefunga mafunzo  ya uongozi, usimamizi na uendeshaji wa shule za msingi yaliyoendeshwa kwa Walimu Wakuu wa Shule za Msingi za Mikoa wa Simiyu, Kigoma, Tanga, Kilimanjaro, Mbeya na Mtwara chini ya mradi wa BOOST na kusimamiwa na Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM).

 

Akizungumza katika ufungaji wa mafunzo hayo, Balozi amewataka walimu hao kwenda kuboresha utendaji kazi katika vituo vyao vya kazi kwa kihakikisha wanasimamia kikamilifu shughuli za ufundishaji na ujifunzaji shuleni kwa ubora.

 

"ADEM imemaliza kazi yake ya kuendesha mafunzo haya kwa walimu wakuu katika Mikoa sita nchini, ni wajibu wa Walimu Wakuu mliopatiwa mafunzo haya kwenda kuyatumia katika utendaji wenu wa kila siku ili kufikia adhma ya Serikali ya kuboresha elimumsingi nchini" Amesema. Balozi

 

Balozi aliwataka Walimu Wakuu kuongoza shule kwa kufuata sheria na taratibu za utumishi wa umma na kusimamia miradi ya elimu wanayotakiwa kusimamia kwa ufanisi kwani kupitia mafunzo hayo wamejengewa uwezo kuhusu usimamizi wa rasilimali za shule hususani fedha na miradi ya ujenzi inayotekelezwa shuleni.

 

Balozi alimalizia kwa kuupongeza uongozi wa ADEM kwa kuendesha mafunzo hayo kwa umahiri mkubwa na kuwataka kuendelea kuendesha mafunzo hayo kwa umahiri huo huo katika Mikoa iliyobaki.

 

Nae Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Elekezi -ADEM Dkt. Alphonce Amuli ameeleza kuwa hadi sasa ADEM imeshatoa mafunzo kwa walimu wakuu 4,522 katika awamu ya kwanza ya mafunzo hayo, na katika awamu hii mafunzo hayo yametolewa kwa Walimu Wakuu 4,620 katika Mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Simiyu, Mbeya, Kigoma na Mtwara kuanzia februari 15 hadi machi 13, 2024.

 

Dkt. Amuli aliwataka walimu kutumia mafunzo hayo katika kuboresha utendaji na usimamizi wa shule ili kuleta tija na thamani ya fedha iliyotumika kuyaendesha ionekane.

 

alisema kuwa Lengo la mafunzo ni kumjengea uwezo Mwalimu Mkuu kutekeleza majukumu yake ya kusimamia shule hususani katika kuhakikisha shughuli za shule zinafanyika kwa ubora na ufanisi unaotakiwa. Mwalimu Mkuu ni mtendaji muhimu katika ngazi ya shule.

 

Dkt. Amuli alisema kuwa baada ya mafunzo hayo, washiriki watafuatiliwa na kupimwa katika maeneo yote waliyowezeshwa,Miongoni mwa viashiria vya utekelezaji wa mafunzo kwa Mwalimu Mkuu ni pamoja na uwepo wa taarifa zifuatazo,Mpango wa Jumla wa Maendeleo ya Shule,Mpango wa kushughulikia malalamiko kwa Watumishi, wanafunzi na jamii,Mpango wa Motisha kwa wafanyakazi na wanafunzi,Miundombinu bora ya shule,Matokeo chanya ya ujifunzaji na ufundishaji shuleni.


Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More